Friday, June 20, 2014

Ndege aliyoizindua Nyalandu mbovu

*Ni zawadi ya Ujerumani kwa ajili ya kupambana na ujangili
*Yadaiwa ipo JNIA kwa miaka mitatu, imepakwa rangi juzi tu
*Haijawahi kuruka tangu itue Dar es Salaam kutoka ughaibuni

NA MWANDISHI WETU, Dar
WAKATI dunia ikiwa katika vita ya kupambana na ujangili, juzi usiku, Waziri wa Maliasili na Utalii, Lazaro Nyalandu alizindua ndege iliyotolewa na Ujerumani kwa ajili ya mapambano hayo.

Ndege hiyo ilizinduliwa mwishoni mwa ziara ya Waziri wa Mambo ya Nje wa Ujerumani Frank-Walter Steinmeier, kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Julius Nyerere (JNIA) jijini Dar es Salaam.
Hata hivyo, taarifa zilizolifikia gazeti hili kutoka kwa vyanzo vyake vya uhakika zimeweka wazi kuwa ndege hiyo inayotarajiwa kutumiwa na Wizara ya Maliasili na Utalii kupambana na ujangili, ni mbovu.
Sherehe za uzinduzi huo zilihudhuriwa na viongozi mbalimbali, watendaji wa wizara husika na waandishi wa habari.
“Ndege hii (iliyozinduliwa), ipo hapa hapa uwanjani (JNIA) kwa kama miaka mitatu hivi; haijawahi kuruka tangu ifike hapa, sasa iweje leo ikabidhiwe kwa serikali kupambana na ujangili? Hapa kuna kitu hakijakaa vyema,” alisema mtoa habari wetu, Ofisa wa Uwanja wa Ndege ambaye ni wazi hatutoweza kuandika jina lake gazetini kwa sasa.
Alisema kilichofanyika kabla ya kuzinduliwa kwa ndege hiyo hapo juzi, ni kupaka rangi iweze kuonekana kama mpya, au walau inaweza kufanya kazi, wakati ukweli wa ndege hiyo unajulikana.
“Kazi inayotarajiwa kwenda kufanywa na ndege hiyo ni kubwa kuliko uwezo wake. Ikitumika, kuna uwezekano mkubwa wa maafa kutokea na Watanzania wenzetu kupoteza maisha.
“Huu sasa ni kuuanika umasikini wa nchi yetu hata pasipo na sababu. Ndege hii haijawahi kufanya safari yoyote kutoka sehemu moja kwenda nyingine. Kwanini maliasili wakubali kupokea ‘kimeo’,” alisema na kuhoji ofisa mwingine uwanjani hapo.
Akizungumza na Raia Tanzania jana, mwanachi mmoja aliishangaa Serikali kushindwa kununua ndege rasmi kwa ajili ya kupambana na majangili, kama kweli inahitajika, badala ya kupokea ndege iliyotelekezwa uwanjani kwa miaka miwili au mitatu.
“Umasikini ni kitu kibaya sana, unaweza kupewa msaada bandia huku unashangilia. Kwa nini wizara isitumie wataalamu wa masuala ya ndege waliopo nchini kuikagua kabla ya kuzinduliwa?,” alihoji.
Hata hivyo, pamoja na unyeti wa suala hili, bado Waziri wa Maliasili na Utalii, Nyalandu na katibu mkuu wake, Maimuna Tarishi, hawakutoa ushirikiano kwa mwandishi wa habari hii.
Nyalandu, alipopigiwa simu ya mkononi kwa mara ya kwanza saa 6.49 mchana, hakupokea simu; na alipoandikiwa ujumbe mfupi wa maandishi dakika chache baadaye, alijibu kwa kifupi ‘I am in a meeting’.
Na alipotafutwa tena saa 8.29 mchana, bado hakupokea na kutuma ujumbe wenye maneno yale yale, kwamba yuko kwenye mkutano.
Wadadisi wa mambo jijini Dar es Salaam, wamekuwa wakihoji uhalali wa kutumia nguvu nyingi kupambana na majangili ambao serikali imeshaitangazia dunia kuwa inawafahamu, na kwamba kinara wao anaishi Arusha.
Mmoja kati yao, aliliambia Raia Tanzania kuwa ni ajabu kwa serikali kupokea zawadi za magari na ndege kwa ajili ya kupambana na majangili wanaofahamika.
 

No comments:

Post a Comment